mtoto.news

Uboreshaji wa Afya, Lishe Bora na Elimu ya Watoto

June 21, 2022

Zaidi ya watoto 8,000 walio chini ya umri wa miaka mitatu wananufaika na mpango wa uhawilishaji wa pesa taslim za Kenya milioni 80 unaofanyiwa majaribio katika kaunti tatu.

Mkurugenzi Msaidizi wa Huduma za Watoto katika idara ya serikali ya Ulinzi wa Jamii, masuala ya wazee na programu maalum Peter Ombasa amesema kuwa, watoto 8,265 wanaochukuliwa kutoka kwa kaya zote katika kaunti hizo tatu wamekuwa wakipokea Sh800 kwa kila mtoto kwa mwezi, tangu kuanzishwa kwa mpango huo nchini mnamo Desemba 2021.

Mpango huo wa mwaka mmoja, uliopewa jina la Universal Child Benefit (UCB) unafanyiwa majaribio katika kaunti ndogo zenye watu wengi zaidi , ambazi ni kaunti ya Kisumu, Embu na Kajiado.

Ombasa aliendelea kusema kuwa mpango huo uliokuwa ukifanyiwa majaribio na Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Watoto (UNICEF) kwa ushirikiano na shirika la Save the Children, Mpango wa Chakula Duniani na serikali ya Kenya unatazamiwa kumalizika Desemba mwaka 2022.

Pamoja na kubainisha kuwa kila mtoto ana haki ya kikatiba ya kupata hifadhi ya jamii, Mkurugenzi huyo alisisitiza haja ya kuboresha matokeo ya watoto kama vile lishe bora, afya na elimu ambayo mpango wa UCB unahakikisha.

Alisisitiza kuwa, watoto, wakiwa kama kizazi kijacho ni kama kitega uchumi cha taifa lolote ambalo likitunzwa vizuri, basi litaweza kutoa faida kubwa na kukuza mtaji wa watu nchini.

Akizungumza wakati wa warsha ya ushirikishwaji wa vyombo vya habari, Ombasa alisema kuwa, mpango huo uliundwa ili kukabiliana na mshtuko kwa watoto walio katika kaya zilizo katika mazingira magumu ili kusaidia kuongeza ustahimilivu wao na pia kutoa jukwaa la utoaji wa pesa za dharura inapohitajika.

Mpango huo ukitekelezwa vyema kote nchini, basi utachangia ukuaji wa uchumi shirikishi kwa kupunguza tofauti zilizopo za kijamii na kuimarisha mshikamano wa kijamii miongoni mwa jamii.

Mpango huo wa majaribio ambao unafadhiliwa na UNICEF unatarajiwa kukabidhiwa kwa serikali kwa ajili ya kuendelea na kuongezwa baada ya kumalizika muda wake Disemba mwaka huu.

Hey, like this? Why not share it with a buddy?

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *